Zaburi 22
Kilio cha uchungu na wimbo wa sifa
Kwa mwimbishaji. Mtindo wa utenzi wa “Kulungu wa Alfajiri”. Zaburi ya Daudi.
1 Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?
Kwa nini uko mbali hivyo kuniokoa?
Mbali hivyo na maneno ya kuugua kwangu?
2 Ee Mungu wangu, ninalia mchana, lakini hunijibu,
hata usiku, sinyamazi.
3 Hata hivyo umesimikwa kwenye kiti cha enzi,
Wewe Uliye Mtakatifu;
wewe ni sifa ya Israeli.*Tafsiri zingine zinasema uketiye juu ya sifa za Israeli.
4 Kwako wewe baba zetu waliweka tumaini lao,
walikutumaini nawe ukawaokoa.
5 Walikulilia wewe na ukawaokoa,
walikutegemea wewe nao hawakuaibika.
6 Mimi ni mnyoo wala si mwanadamu,
wanaume wamenibeza, na watu wamenidharau.
7 Wote wanaoniona wananidhihaki;
wananivurumishia matusi, wakitikisa vichwa vyao:
8 Wanasema, “Amtegemea Mwenyezi Mungu,
basi Mwenyezi Mungu na amwokoe.
Amkomboe basi, kwa maana
anapendezwa naye.”
9 Hata hivyo ulinitoa tumboni,
ukanifanya nikutegemee,
hata nilipokuwa ninanyonya
matiti ya mama yangu.
10 Nimekabidhiwa kwako tangu kuzaliwa,
toka tumboni mwa mama yangu
umekuwa Mungu wangu.
11 Usiwe mbali nami,
kwa maana shida iko karibu
na hakuna wa kunisaidia.
12 Mafahali wengi wamenizunguka,
mafahali wa Bashani wenye nguvu
wamenizingira.
13 Simba wanaonguruma na kurarua mawindo
wanapanua vinywa vyao dhidi yangu.
14 Nimemiminwa kama maji,
mifupa yangu yote imeteguka viungoni.
Moyo wangu umegeuka kuwa nta,
umeyeyuka ndani yangu.
15 Nguvu zangu zimekauka kama kigae,
ulimi wangu umegandamana
na kaakaa la kinywa changu,
kwa sababu umenilaza
katika mavumbi ya kifo.
16 Mbwa wamenizunguka,
kundi la watu waovu limenizingira;
wamenidunga mikono na miguu.
17 Naweza kuhesabu mifupa yangu yote,
watu wananikodolea macho na kunisimanga.
18 Wanagawana nguo zangu,
na vazi langu wanalipigia kura.
19 Lakini wewe, Ee Mwenyezi Mungu,
usiwe mbali.
Ee Nguvu yangu,
uje haraka unisaidie.
20 Okoa maisha yangu na upanga,
uhai wangu wa thamani kutoka nguvu za mbwa.
21 Niokoe kutoka kinywani mwa simba,
niokoe kutoka pembe za nyati.
22 Nitalitangaza jina lako kwa ndugu zangu,
katika kusanyiko nitakusifu wewe.
23 Ninyi ambao mnamcha Mwenyezi Mungu, msifuni!
Ninyi nyote wazao wa Yakobo, mheshimuni yeye!
Mcheni yeye, ninyi wazao wa Israeli!
24 Kwa maana hakupuuza wala kudharau
mateso ya aliyeteswa;
hakumficha uso wake
bali alisikiliza kilio chake.
25 Kwako wewe hutoka kiini cha sifa zangu katika kusanyiko kubwa,
nitatimiza nadhiri zangu mbele ya wale wanaokucha wewe.
26 Maskini watakula na kushiba,
wale wanaomtafuta Mwenyezi Mungu watamsifu:
mioyo yenu na iishi milele!
27 Miisho yote ya dunia itakumbuka
na kumgeukia Mwenyezi Mungu,
nazo jamaa zote za mataifa
zitasujudu mbele zake,
28 kwa maana ufalme ni wa Mwenyezi Mungu
naye huyatawala mataifa.
29 Matajiri wote wa dunia watasherehekea na kuabudu.
Wote wanaoshuka mavumbini
watapiga magoti mbele yake,
wote ambao hawawezi
kudumisha uhai wao.
30 Wazao wa baadaye watamtumikia yeye;
vizazi vijavyo vitajulishwa habari za Bwana.
31 Watatangaza haki yake kwa watu
ambao hawajazaliwa bado,
kwa maana yeye ametenda hili.