Zaburi 23
Mwenyezi Mungu mchungaji wetu 
 Zaburi ya Daudi. 
  1 Mwenyezi Mungu ndiye mchungaji wangu,  
sitapungukiwa na kitu.   
 2 Hunilaza katika malisho  
ya majani mabichi,  
kando ya maji matulivu huniongoza,   
 3 hunihuisha nafsi yangu.  
Huniongoza katika njia za haki  
kwa ajili ya jina lake.   
 4 Hata nikipita katikati  
ya bonde la uvuli wa mauti,  
sitaogopa mabaya,  
kwa maana wewe upo pamoja nami;  
fimbo yako na mkongojo wako  
vyanifariji.   
 5 Waandaa meza mbele yangu  
machoni pa adui zangu.  
Umenipaka mafuta kichwani pangu,  
kikombe changu kinafurika.   
 6 Hakika wema na upendo vitanifuata  
siku zote za maisha yangu,  
nami nitakaa nyumbani mwa Mwenyezi Mungu  
milele.