Zaburi 28
Kuomba msaada 
 Zaburi ya Daudi. 
  1 Ninakuita wewe, Ee Mwenyezi Mungu, Mwamba wangu;  
usikatae kunisikiliza.  
Kwa sababu ukinyamaza  
nitafanana na walioshuka shimoni.   
 2 Sikia kilio changu nikikuomba unihurumie,  
ninapokuita ili unisaidie,  
ninapoinua mikono yangu kuelekea  
Patakatifu pa Patakatifu pako.   
 3 Usiniburute pamoja na waovu,  
pamoja na hao watendao mabaya,  
ambao huzungumza na majirani zao maneno mazuri,  
lakini mioyoni mwao wameficha chuki.   
 4 Walipe sawasawa na matendo yao,  
sawasawa na matendo yao maovu;  
walipe sawasawa na kazi za mikono yao,  
uwalipe wanavyostahili.   
 5 Kwa kuwa hawaheshimu kazi za Mwenyezi Mungu,  
na yale ambayo mikono yake imetenda,  
atawabomoa na kamwe  
hatawajenga tena.   
 6 Ahimidiwe Mwenyezi Mungu,  
kwa maana amesikia kilio changu  
nikimwomba anihurumie.   
 7 Mwenyezi Mungu ni nguvu zangu na ngao yangu,  
moyo wangu umemtumaini yeye,  
nami nimesaidiwa.  
Moyo wangu unarukaruka kwa furaha  
nami nitamshukuru kwa wimbo.   
 8 Mwenyezi Mungu ni nguvu ya watu wake,  
ngome ya wokovu kwa mpakwa mafuta wake.   
 9 Waokoe watu wako na uubariki urithi wako;  
uwe mchungaji wao na uwabebe milele.