Zaburi 29
Sauti ya Mwenyezi Mungu wakati wa dhoruba 
 Zaburi ya Daudi. 
  1 Mpeni Mwenyezi Mungu, enyi mashujaa,  
mpeni Mwenyezi Mungu utukufu na nguvu.   
 2 Mpeni Mwenyezi Mungu utukufu unaostahili jina lake;  
mwabuduni Mwenyezi Mungu katika uzuri wa utakatifu wake.   
 3 Sauti ya Mwenyezi Mungu iko juu ya maji;  
Mungu wa utukufu hupiga radi,  
Mwenyezi Mungu hupiga radi juu ya maji makuu.   
 4 Sauti ya Mwenyezi Mungu ina nguvu;  
sauti ya Mwenyezi Mungu ni tukufu.   
 5 Sauti ya Mwenyezi Mungu huvunja mierezi;  
Mwenyezi Mungu huvunja vipande vipande  
mierezi ya Lebanoni.   
 6 Hufanya Lebanoni irukaruke kama ndama,  
Sirioni*yaani Mlima Hermoni urukaruke kama mwana nyati.   
 7 Sauti ya Mwenyezi Mungu hupiga  
kwa miali ya radi.   
 8 Sauti ya Mwenyezi Mungu hutikisa jangwa;  
Mwenyezi Mungu hutikisa Jangwa la Kadeshi.   
 9 Sauti ya Mwenyezi Mungu huzalisha ayala,  
na huuacha msitu wazi.  
Hekaluni mwake wote wasema,  
“Utukufu!”   
 10 Mwenyezi Mungu huketi akiwa ametawazwa juu ya gharika;  
Mwenyezi Mungu ametawazwa kuwa Mfalme milele.   
 11 Mwenyezi Mungu huwapa watu wake nguvu;  
Mwenyezi Mungu huwabariki watu wake kwa kuwapa amani.