Zaburi 43
Maombi ya mtu aliye uhamishoni yanaendelea 
  1 Ee Mungu unihukumu,  
nitetee dhidi ya taifa lisilomcha Mungu,  
niokoe na watu wadanganyifu na waovu.   
 2 Wewe ni Mungu ngome yangu.  
Kwa nini umenikataa?  
Kwa nini niendelee kuomboleza,  
nikidhulumiwa na adui?   
 3 Tuma hima nuru yako na kweli yako viniongoze;  
na vinilete hadi mlima wako mtakatifu,  
mahali unapoishi.   
 4 Ndipo nitaenda madhabahuni pa Mungu,  
kwa Mungu, furaha yangu na shangwe yangu.  
Nitakusifu kwa kinubi,  
Ee Mungu, Mungu wangu.   
 5 Ee nafsi yangu, kwa nini unasononeka?  
Kwa nini unafadhaika hivyo ndani yangu?  
Weka tumaini lako kwa Mungu,  
kwa sababu bado nitamsifu  
Mwokozi wangu na Mungu wangu.