Zaburi 61
Kuomba ulinzi
Kwa mwimbishaji. Kwa ala za nyuzi za uimbaji. Zaburi ya Daudi.
1 Ee Mungu, sikia kilio changu,
usikilize maombi yangu.
2 Kutoka miisho ya dunia ninakuita,
ninakuita huku moyo wangu unadhoofika;
uniongoze kwenye mwamba
ulio juu kuniliko.
3 Kwa kuwa umekuwa kimbilio langu,
ngome imara dhidi ya adui.
4 Natamani kukaa kwenye hema lako milele,
na kukimbilia chini ya uvuli wa mabawa yako.
5 Ee Mungu, kwa kuwa umesikia nadhiri zangu,
umenipa urithi wa wale wanaoliogopa jina lako.
6 Mwongezee mfalme siku za maisha yake,
miaka yake kwa vizazi vingi.
7 Mtawaze mbele za Mungu milele;
amuru upendo wako na uaminifu wako vimlinde.
8 Ndipo daima nitaliimbia sifa jina lako
na kuzitimiza nadhiri zangu siku baada ya siku.