Zaburi 61
Kuomba ulinzi 
 Kwa mwimbishaji. Kwa ala za nyuzi za uimbaji. Zaburi ya Daudi. 
  1 Ee Mungu, sikia kilio changu,  
usikilize maombi yangu.   
 2 Kutoka miisho ya dunia ninakuita,  
ninakuita huku moyo wangu unadhoofika;  
uniongoze kwenye mwamba  
ulio juu kuniliko.   
 3 Kwa kuwa umekuwa kimbilio langu,  
ngome imara dhidi ya adui.   
 4 Natamani kukaa kwenye hema lako milele,  
na kukimbilia chini ya uvuli wa mabawa yako.   
 5 Ee Mungu, kwa kuwa umesikia nadhiri zangu,  
umenipa urithi wa wale wanaoliogopa jina lako.   
 6 Mwongezee mfalme siku za maisha yake,  
miaka yake kwa vizazi vingi.   
 7 Mtawaze mbele za Mungu milele;  
amuru upendo wako na uaminifu wako vimlinde.   
 8 Ndipo daima nitaliimbia sifa jina lako  
na kuzitimiza nadhiri zangu siku baada ya siku.