Zaburi 62
Mwenyezi Mungu kimbilio la pekee 
 Kwa mwimbishaji. Mtindo wa Yeduthuni. Zaburi ya Daudi. 
  1 Nafsi yangu inapata pumziko kwa Mungu peke yake;  
wokovu wangu watoka kwake.   
 2 Yeye peke yake ndiye mwamba wangu na wokovu wangu;  
yeye ni ngome yangu, sitatikisika kamwe.   
 3 Mtanishambulia hadi lini?  
Je, ninyi nyote mtanitupa chini:  
Mimi niliye kama ukuta ulioinama,  
kama uzio unaotikisika?   
 4 Walikusudia kikamilifu kumwangusha  
toka mahali pake pa fahari;  
wanafurahia uongo.  
Kwa vinywa vyao hubariki,  
lakini ndani ya mioyo yao hulaani.   
 5 Ee nafsi yangu, upumzike, kwa Mungu peke yake,  
tumaini langu latoka kwake.   
 6 Yeye peke yake ndiye mwamba wangu na wokovu wangu;  
ndiye ngome yangu, sitatikisika.   
 7 Wokovu wangu na heshima yangu viko kwa Mungu,  
ndiye mwamba wangu wenye nguvu  
na kimbilio langu.   
 8 Enyi watu, mtumainini yeye wakati wote,  
miminieni mioyo yenu kwake,  
kwa kuwa Mungu ni kimbilio letu.   
 9 Binadamu wa ngazi ya chini ni pumzi tu,  
nao wa ngazi ya juu ni uongo tu;  
wakipimwa kwenye mizani, si chochote;  
wote kwa pamoja ni pumzi tu.   
 10 Usitumainie udhalimu,  
wala ujivune kwa vitu vya wizi;  
ingawa utajiri wako utaongezeka,  
usiuweke moyoni mwako.   
 11 Jambo moja Mungu amelisema,  
mambo mawili nimeyasikia:  
kwamba, Ee Mungu,  
wewe una nguvu,   
 12 na kwamba, Ee Bwana,  
wewe ni mwenye upendo.  
Hakika utampa kila mtu thawabu  
kwa kadiri ya alivyotenda.