Zaburi 62
Mwenyezi Mungu kimbilio la pekee
Kwa mwimbishaji. Mtindo wa Yeduthuni. Zaburi ya Daudi.
1 Nafsi yangu inapata pumziko kwa Mungu peke yake;
wokovu wangu watoka kwake.
2 Yeye peke yake ndiye mwamba wangu na wokovu wangu;
yeye ni ngome yangu, sitatikisika kamwe.
3 Mtanishambulia hadi lini?
Je, ninyi nyote mtanitupa chini:
Mimi niliye kama ukuta ulioinama,
kama uzio unaotikisika?
4 Walikusudia kikamilifu kumwangusha
toka mahali pake pa fahari;
wanafurahia uongo.
Kwa vinywa vyao hubariki,
lakini ndani ya mioyo yao hulaani.
5 Ee nafsi yangu, upumzike, kwa Mungu peke yake,
tumaini langu latoka kwake.
6 Yeye peke yake ndiye mwamba wangu na wokovu wangu;
ndiye ngome yangu, sitatikisika.
7 Wokovu wangu na heshima yangu viko kwa Mungu,
ndiye mwamba wangu wenye nguvu
na kimbilio langu.
8 Enyi watu, mtumainini yeye wakati wote,
miminieni mioyo yenu kwake,
kwa kuwa Mungu ni kimbilio letu.
9 Binadamu wa ngazi ya chini ni pumzi tu,
nao wa ngazi ya juu ni uongo tu;
wakipimwa kwenye mizani, si chochote;
wote kwa pamoja ni pumzi tu.
10 Usitumainie udhalimu,
wala ujivune kwa vitu vya wizi;
ingawa utajiri wako utaongezeka,
usiuweke moyoni mwako.
11 Jambo moja Mungu amelisema,
mambo mawili nimeyasikia:
kwamba, Ee Mungu,
wewe una nguvu,
12 na kwamba, Ee Bwana,
wewe ni mwenye upendo.
Hakika utampa kila mtu thawabu
kwa kadiri ya alivyotenda.