Zaburi 65
Kusifu na kushukuru 
 Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi. Wimbo. 
  1 Ee Mungu, sifa zakungojea katika Sayuni;  
kwako wewe nadhiri zetu zitatimizwa.   
 2 Ewe usikiaye maombi,  
watu wote watakuja kwako wewe.   
 3 Tulipokuwa tumefunikwa kabisa na dhambi,  
wewe ulisamehe makosa yetu.   
 4 Heri wale uliowachagua  
na kuwaleta karibu ili waishi katika nyua zako!  
Tunashibishwa kwa mema ya nyumba yako,  
mema ya Hekalu lako takatifu.   
 5 Unatujibu kwa matendo ya kushangaza ya haki,  
Ee Mungu Mwokozi wetu,  
tumaini la miisho yote ya duniani  
na la bahari zilizo mbali sana,   
 6 uliyeumba milima kwa uwezo wako,  
ukiwa umejivika nguvu,   
 7 uliyenyamazisha dhoruba za bahari,  
ngurumo za mawimbi yake,  
na ghasia za mataifa.   
 8 Wale wanaoishi mbali sana  
wanaogopa maajabu yako,  
kule asubuhi ipambazukiapo  
na kule jioni inakofifilia  
umeziita nyimbo za furaha.   
 9 Waitunza nchi na kuinyeshea,  
waitajirisha kwa wingi.  
Vijito vya Mungu vimejaa maji  
ili kuwapa watu nafaka,  
kwa maana wewe umeviamuru.   
 10 Umeilowesha mifereji yake  
na kusawazisha kingo zake;  
umeilainisha kwa manyunyu  
na kuibariki mimea yake.   
 11 Umeuvika mwaka taji la baraka,  
magari yako yanafurika kwa wingi.   
 12 Mbuga za majani za jangwani umezineemesha;  
vilima vimevikwa furaha.   
 13 Malisho yamejaa makundi ya wanyama,  
na mabonde yamepambwa kwa mavuno;  
vyote vinashangilia kwa furaha na kuimba.