Zaburi 64
Kuomba ulinzi dhidi ya adui
Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi.
1 Ee Mungu, unisikie ninapoeleza lalamiko langu,
uyahifadhi maisha yangu kutokana na vitisho vya adui.
2 Unifiche kutokana na njama za waovu,
kutokana na fitina za kundi la watenda maovu.
3 Wananoa ndimi zao kama panga
na kuelekeza maneno yao kama mishale ya kufisha.
4 Hurusha mishale kutoka mavizio kwa mtu asiye na hatia,
humrushia ghafula bila woga.
5 Kila mmoja humtia moyo mwenzake
katika mipango mibaya;
huzungumza kuhusu kuficha mitego yao,
nao husema, “Ni nani ataiona?”
6 Hupanga njama la dhuluma na kusema,
“Tumebuni mpango mkamilifu!”
Hakika nia na moyo wa mwanadamu vina hila.
7 Bali Mungu atawapiga kwa mishale,
nao ghafula wataangushwa.
8 Atageuza ndimi zao wenyewe dhidi yao
na kuwaleta kwenye maangamizi;
wote wawaonao watatikisa vichwa vyao
kwa dharau.
9 Wanadamu wote wataogopa,
watatangaza kazi za Mungu
na kutafakari yale aliyoyatenda.
10 Wenye haki na wafurahi katika Mwenyezi Mungu,
na wakimbilie kwake;
wanyofu wote wa moyo na wamsifu yeye!