Zaburi 64
Kuomba ulinzi dhidi ya adui 
 Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi. 
  1 Ee Mungu, unisikie ninapoeleza lalamiko langu,  
uyahifadhi maisha yangu kutokana na vitisho vya adui.   
 2 Unifiche kutokana na njama za waovu,  
kutokana na fitina za kundi la watenda maovu.   
 3 Wananoa ndimi zao kama panga  
na kuelekeza maneno yao kama mishale ya kufisha.   
 4 Hurusha mishale kutoka mavizio kwa mtu asiye na hatia,  
humrushia ghafula bila woga.   
 5 Kila mmoja humtia moyo mwenzake  
katika mipango mibaya;  
huzungumza kuhusu kuficha mitego yao,  
nao husema, “Ni nani ataiona?”   
 6 Hupanga njama la dhuluma na kusema,  
“Tumebuni mpango mkamilifu!”  
Hakika nia na moyo wa mwanadamu vina hila.   
 7 Bali Mungu atawapiga kwa mishale,  
nao ghafula wataangushwa.   
 8 Atageuza ndimi zao wenyewe dhidi yao  
na kuwaleta kwenye maangamizi;  
wote wawaonao watatikisa vichwa vyao  
kwa dharau.   
 9 Wanadamu wote wataogopa,  
watatangaza kazi za Mungu  
na kutafakari yale aliyoyatenda.   
 10 Wenye haki na wafurahi katika Mwenyezi Mungu,  
na wakimbilie kwake;  
wanyofu wote wa moyo na wamsifu yeye!