Zaburi 67
Mataifa wahimizwa kumsifu Mwenyezi Mungu 
 Kwa mwimbishaji. Na ala za nyuzi za muziki. Zaburi. Wimbo. 
  1 Mungu aturehemu na kutubariki,  
na kutuangazia nuru za uso wake,   
 2 ili njia zako zijulikane duniani,  
wokovu wako katikati ya mataifa yote.   
 3 Ee Mungu, mataifa na wakusifu,  
mataifa yote na wakusifu.   
 4 Mataifa yote wafurahi na kuimba kwa shangwe,  
kwa kuwa unatawala watu kwa haki  
na kuongoza mataifa ya dunia.   
 5 Ee Mungu, mataifa na wakusifu,  
mataifa yote na wakusifu.   
 6 Ndipo nchi itatoa mazao yake,  
naye Mungu, Mungu wetu, atatubariki.   
 7 Mungu atatubariki  
na miisho yote ya dunia itamcha yeye.