Zaburi 93
Mwenyezi Mungu ni mkuu 
  1 Mwenyezi Mungu anatawala, amejivika utukufu;  
Mwenyezi Mungu amejivika utukufu  
tena amejivika nguvu.  
Dunia imewekwa imara,  
haitaondoshwa.   
 2 Kiti chako cha enzi kimekuwa thabiti tangu zamani;  
wewe umekuwa tangu milele.   
 3 Bahari zimepaza, Ee Mwenyezi Mungu,  
bahari zimepaza sauti zake;  
bahari zimepaza sauti za mawimbi yake.   
 4 Yeye ni mkuu kuliko ngurumo ya maji makuu,  
ni mkuu kuliko mawimbi ya bahari:  
Mwenyezi Mungu aishiye juu sana ni mkuu.   
 5 Ee Mwenyezi Mungu, sheria zako ni imara;  
utakatifu umepamba nyumba yako  
pasipo mwisho.