Zaburi 96
Mwenyezi Mungu Mfalme mkuu
(1 Nyakati 16:23-33)
Mwimbieni Mwenyezi Mungu wimbo mpya;
mwimbieni Mwenyezi Mungu dunia yote.
Mwimbieni Mwenyezi Mungu, lisifuni jina lake;
tangazeni wokovu wake siku baada ya siku.
Tangazeni utukufu wake katika mataifa,
matendo yake ya ajabu miongoni mwa mataifa yote.
 
Kwa kuwa Mwenyezi Mungu ni mkuu mwenye kustahili kusifiwa kuliko wote;
yeye ni wa kuogopwa kuliko miungu yote.
Kwa maana miungu yote ya mataifa ni sanamu,
lakini Mwenyezi Mungu aliziumba mbingu.
Fahari na enzi viko mbele yake;
nguvu na utukufu vimo patakatifu pake.
 
Mpeni Mwenyezi Mungu, enyi jamaa za mataifa,
mpeni Mwenyezi Mungu utukufu na nguvu.
Mpeni Mwenyezi Mungu utukufu unaostahili jina lake;
leteni sadaka na mje katika nyua zake.
Mwabuduni Mwenyezi Mungu katika uzuri wa utakatifu wake;
dunia yote na itetemeke mbele zake.
 
10 Semeni katika mataifa kwamba, “Mwenyezi Mungu anatawala.”
Ulimwengu ameuweka imara, hauwezi kusogezwa;
atawahukumu watu kwa uadilifu.
11 Mbingu na zishangilie, nchi na ifurahi;
bahari na ivume, na vyote vilivyo ndani yake;
12 mashamba na yashangilie,
pamoja na vyote vilivyomo.
Kisha miti yote ya msituni itaimba kwa furaha;
13 itaimba mbele za Mwenyezi Mungu kwa maana anakuja,
anakuja kuihukumu dunia.
Ataihukumu dunia kwa haki,
na mataifa katika kweli yake.