Zaburi 96
Mwenyezi Mungu Mfalme mkuu 
 (1 Nyakati 16:23-33)  
 1 Mwimbieni Mwenyezi Mungu wimbo mpya;  
mwimbieni Mwenyezi Mungu dunia yote.   
 2 Mwimbieni Mwenyezi Mungu, lisifuni jina lake;  
tangazeni wokovu wake siku baada ya siku.   
 3 Tangazeni utukufu wake katika mataifa,  
matendo yake ya ajabu miongoni mwa mataifa yote.   
 4 Kwa kuwa Mwenyezi Mungu ni mkuu mwenye kustahili kusifiwa kuliko wote;  
yeye ni wa kuogopwa kuliko miungu yote.   
 5 Kwa maana miungu yote ya mataifa ni sanamu,  
lakini Mwenyezi Mungu aliziumba mbingu.   
 6 Fahari na enzi viko mbele yake;  
nguvu na utukufu vimo patakatifu pake.   
 7 Mpeni Mwenyezi Mungu, enyi jamaa za mataifa,  
mpeni Mwenyezi Mungu utukufu na nguvu.   
 8 Mpeni Mwenyezi Mungu utukufu unaostahili jina lake;  
leteni sadaka na mje katika nyua zake.   
 9 Mwabuduni Mwenyezi Mungu katika uzuri wa utakatifu wake;  
dunia yote na itetemeke mbele zake.   
 10 Semeni katika mataifa kwamba, “Mwenyezi Mungu anatawala.”  
Ulimwengu ameuweka imara, hauwezi kusogezwa;  
atawahukumu watu kwa uadilifu.   
 11 Mbingu na zishangilie, nchi na ifurahi;  
bahari na ivume, na vyote vilivyo ndani yake;   
 12 mashamba na yashangilie,  
pamoja na vyote vilivyomo.  
Kisha miti yote ya msituni itaimba kwa furaha;   
 13 itaimba mbele za Mwenyezi Mungu kwa maana anakuja,  
anakuja kuihukumu dunia.  
Ataihukumu dunia kwa haki,  
na mataifa katika kweli yake.