Zaburi 98
Mwenyezi Mungu Mtawala wa dunia 
 Zaburi. 
  1 Mwimbieni Mwenyezi Mungu wimbo mpya,  
kwa maana ametenda mambo ya ajabu;  
kitanga chake cha kuume na mkono wake mtakatifu  
umemfanyia wokovu.   
 2 Mwenyezi Mungu ameufanya wokovu wake ujulikane  
na amedhihirisha haki yake kwa mataifa.   
 3 Ameukumbuka upendo wake  
na uaminifu wake kwa nyumba ya Israeli;  
miisho yote ya dunia imeuona  
wokovu wa Mungu wetu.   
 4 Mpigieni Mwenyezi Mungu kelele za shangwe, dunia yote,  
ipaze sauti kwa nyimbo za shangwe na vinanda;   
 5 mwimbieni Mwenyezi Mungu kwa kinubi,  
kwa kinubi na sauti za kuimba,   
 6 kwa tarumbeta na mvumo wa baragumu za pembe za kondoo dume:  
shangilieni kwa furaha mbele za Mwenyezi Mungu, aliye Mfalme.   
 7 Bahari na ivume na kila kilicho ndani yake,  
dunia na wote wanaoishi ndani yake.   
 8 Mito na ipige makofi,  
milima na iimbe pamoja kwa furaha,   
 9 vyote na viimbe mbele za Mwenyezi Mungu,  
kwa maana yuaja kuhukumu dunia.  
Atahukumu dunia kwa haki  
na mataifa kwa haki.