Zaburi 98
Mwenyezi Mungu Mtawala wa dunia
Zaburi.
1 Mwimbieni Mwenyezi Mungu wimbo mpya,
kwa maana ametenda mambo ya ajabu;
kitanga chake cha kuume na mkono wake mtakatifu
umemfanyia wokovu.
2 Mwenyezi Mungu ameufanya wokovu wake ujulikane
na amedhihirisha haki yake kwa mataifa.
3 Ameukumbuka upendo wake
na uaminifu wake kwa nyumba ya Israeli;
miisho yote ya dunia imeuona
wokovu wa Mungu wetu.
4 Mpigieni Mwenyezi Mungu kelele za shangwe, dunia yote,
ipaze sauti kwa nyimbo za shangwe na vinanda;
5 mwimbieni Mwenyezi Mungu kwa kinubi,
kwa kinubi na sauti za kuimba,
6 kwa tarumbeta na mvumo wa baragumu za pembe za kondoo dume:
shangilieni kwa furaha mbele za Mwenyezi Mungu, aliye Mfalme.
7 Bahari na ivume na kila kilicho ndani yake,
dunia na wote wanaoishi ndani yake.
8 Mito na ipige makofi,
milima na iimbe pamoja kwa furaha,
9 vyote na viimbe mbele za Mwenyezi Mungu,
kwa maana yuaja kuhukumu dunia.
Atahukumu dunia kwa haki
na mataifa kwa haki.