Zaburi 99
Mwenyezi Mungu Mfalme mtakatifu 
  1 Mwenyezi Mungu anatawala,  
mataifa na yatetemeke;  
anakalia kiti cha enzi katikati ya makerubi,  
dunia na itikisike.   
 2 Mwenyezi Mungu ni mkuu katika Sayuni;  
ametukuzwa juu ya mataifa yote.   
 3 Wanalisifu jina lako ambalo ni kuu na la kuogopwa:  
yeye ni mtakatifu!   
 4 Mfalme ni mwenye nguvu na hupenda haki,  
wewe umethibitisha adili;  
katika Yakobo umefanya  
yaliyo haki na sawa.   
 5 Mtukuzeni Mwenyezi Mungu, Mungu wetu,  
na mkaabudu katika mahali pa kuwekea miguu yake;  
yeye ni mtakatifu.   
 6 Musa na Haruni walikuwa miongoni mwa makuhani wake,  
Samweli alikuwa miongoni mwa walioliitia jina lake;  
walimwita Mwenyezi Mungu,  
naye aliwajibu.   
 7 Alizungumza nao kutoka nguzo ya wingu;  
walizishika sheria zake na amri alizowapa.   
 8 Ee Mwenyezi Mungu, Mungu wetu,  
ndiwe uliyewajibu,  
kwa Israeli ulikuwa Mungu mwenye kusamehe,  
ingawa uliadhibu matendo yao mabaya.   
 9 Mtukuzeni Mwenyezi Mungu, Mungu wetu,  
mwabuduni kwenye mlima wake mtakatifu,  
kwa maana Mwenyezi Mungu, Mungu wetu, ni mtakatifu.