Zaburi 101
Ahadi ya kuishi kwa uadilifu na kwa haki 
 Zaburi ya Daudi. 
  1 Nitaimba kuhusu upendo wako na haki yako;  
kwako wewe, Ee Mwenyezi Mungu, nitaimba sifa.   
 2 Nitazingatia kuishi maisha yasiyo na lawama:  
utakuja kwangu lini?  
Nitatembea nyumbani mwangu  
kwa moyo usio na lawama.   
 3 Sitaweka mbele ya macho yangu  
kitu kiovu.  
Ninayachukia matendo ya watu wasio na imani;  
hawatashikamana nami.   
 4 Moyo wa ukaidi utakuwa mbali nami;  
nitajitenga na kila ubaya.   
 5 Kila amsingiziaye jirani yake kwa siri,  
huyo nitamnyamazisha;  
mwenye macho ya dharau na moyo wa kiburi  
huyo sitamvumilia.   
 6 Macho yangu yatawaelekea waaminifu katika nchi,  
ili waweze kuishi pamoja nami;  
yeye ambaye moyo wake hauna lawama  
atanitumikia.   
 7 Mdanganyifu hatakaa  
nyumbani mwangu,  
yeye asemaye kwa uongo  
hatasimama mbele yangu.   
 8 Kila asubuhi nitawanyamazisha  
waovu wote katika nchi;  
nitamkatilia mbali kila mtenda maovu  
kutoka mji wa Mwenyezi Mungu.