Zaburi 101
Ahadi ya kuishi kwa uadilifu na kwa haki
Zaburi ya Daudi.
1 Nitaimba kuhusu upendo wako na haki yako;
kwako wewe, Ee Mwenyezi Mungu, nitaimba sifa.
2 Nitazingatia kuishi maisha yasiyo na lawama:
utakuja kwangu lini?
Nitatembea nyumbani mwangu
kwa moyo usio na lawama.
3 Sitaweka mbele ya macho yangu
kitu kiovu.
Ninayachukia matendo ya watu wasio na imani;
hawatashikamana nami.
4 Moyo wa ukaidi utakuwa mbali nami;
nitajitenga na kila ubaya.
5 Kila amsingiziaye jirani yake kwa siri,
huyo nitamnyamazisha;
mwenye macho ya dharau na moyo wa kiburi
huyo sitamvumilia.
6 Macho yangu yatawaelekea waaminifu katika nchi,
ili waweze kuishi pamoja nami;
yeye ambaye moyo wake hauna lawama
atanitumikia.
7 Mdanganyifu hatakaa
nyumbani mwangu,
yeye asemaye kwa uongo
hatasimama mbele yangu.
8 Kila asubuhi nitawanyamazisha
waovu wote katika nchi;
nitamkatilia mbali kila mtenda maovu
kutoka mji wa Mwenyezi Mungu.