Zaburi 120
Kuomba msaada dhidi ya wadanganyifu
Wimbo wa kwenda juu.
Katika dhiki yangu namwita Mwenyezi Mungu,
naye hunijibu.
Ee Mwenyezi Mungu, uniokoe kutoka midomo ya uongo
na ndimi za udanganyifu.
 
Atakufanyia nini,
au akufanyie nini zaidi, ewe ulimi mdanganyifu?
Atakuadhibu kwa mishale mikali ya shujaa,
kwa makaa yanayowaka ya mti wa mretemu.
 
Ole wangu kwa kuwa naishi Mesheki,
kwamba naishi katikati ya mahema ya Kedari!
Nimeishi muda mrefu mno
miongoni mwa wale wanaochukia amani.
Mimi ni mtu wa amani;
lakini ninaposema, wao wanataka vita.