Zaburi 121
Mwenyezi Mungu mlinzi wetu 
 Wimbo wa kwenda juu. 
  1 Nayainua macho yangu natazama milima:  
msaada wangu utatoka wapi?   
 2 Msaada wangu hutoka kwa Mwenyezi Mungu,  
Muumba wa mbingu na dunia.   
 3 Hatauacha mguu wako uteleze,  
yeye akulindaye hatasinzia,   
 4 hakika, yeye alindaye Israeli  
hatasinzia wala hatalala usingizi.   
 5 Mwenyezi Mungu anakulinda,  
Mwenyezi Mungu ni uvuli wako mkono wako wa kuume,   
 6 jua halitakudhuru mchana,  
wala mwezi wakati wa usiku.   
 7 Mwenyezi Mungu atakukinga na madhara yote,  
atayalinda maisha yako,   
 8 Mwenyezi Mungu atakulinda unapoingia na unapotoka,  
tangu sasa na hata milele.