Zaburi 121
Mwenyezi Mungu mlinzi wetu
Wimbo wa kwenda juu.
1 Nayainua macho yangu natazama milima:
msaada wangu utatoka wapi?
2 Msaada wangu hutoka kwa Mwenyezi Mungu,
Muumba wa mbingu na dunia.
3 Hatauacha mguu wako uteleze,
yeye akulindaye hatasinzia,
4 hakika, yeye alindaye Israeli
hatasinzia wala hatalala usingizi.
5 Mwenyezi Mungu anakulinda,
Mwenyezi Mungu ni uvuli wako mkono wako wa kuume,
6 jua halitakudhuru mchana,
wala mwezi wakati wa usiku.
7 Mwenyezi Mungu atakukinga na madhara yote,
atayalinda maisha yako,
8 Mwenyezi Mungu atakulinda unapoingia na unapotoka,
tangu sasa na hata milele.