Zaburi 122
Sifa kwa Yerusalemu 
 Wimbo wa kwenda juu. Wa Daudi. 
  1 Nilishangilia pamoja na wale walioniambia,  
“Twende nyumbani mwa Mwenyezi Mungu.”   
 2 Ee Yerusalemu, miguu yetu imesimama  
malangoni mwako.   
 3 Yerusalemu imejengwa vyema kama mji  
ulioshikamana pamoja.   
 4 Huko ndiko makabila hukwea,  
makabila ya Mwenyezi Mungu,  
kulisifu jina la Mwenyezi Mungu kulingana na maagizo  
waliopewa Israeli.   
 5 Huko viti vya hukumu hukaa,  
viti vya ufalme vya nyumba ya Daudi.   
 6 Omba kwa ajili ya amani ya Yerusalemu:  
“Wote wanaokupenda na wawe salama.   
 7 Amani na iwe ndani ya kuta zako,  
na usalama ndani ya ngome zako.”   
 8 Kwa ajili ya ndugu na rafiki zangu,  
nitasema, “Amani iwe ndani yako.”   
 9 Kwa ajili ya nyumba ya Mwenyezi Mungu, Mungu wetu,  
nitatafuta mafanikio yako.