Zaburi 122
Sifa kwa Yerusalemu
Wimbo wa kwenda juu. Wa Daudi.
1 Nilishangilia pamoja na wale walioniambia,
“Twende nyumbani mwa Mwenyezi Mungu.”
2 Ee Yerusalemu, miguu yetu imesimama
malangoni mwako.
3 Yerusalemu imejengwa vyema kama mji
ulioshikamana pamoja.
4 Huko ndiko makabila hukwea,
makabila ya Mwenyezi Mungu,
kulisifu jina la Mwenyezi Mungu kulingana na maagizo
waliopewa Israeli.
5 Huko viti vya hukumu hukaa,
viti vya ufalme vya nyumba ya Daudi.
6 Omba kwa ajili ya amani ya Yerusalemu:
“Wote wanaokupenda na wawe salama.
7 Amani na iwe ndani ya kuta zako,
na usalama ndani ya ngome zako.”
8 Kwa ajili ya ndugu na rafiki zangu,
nitasema, “Amani iwe ndani yako.”
9 Kwa ajili ya nyumba ya Mwenyezi Mungu, Mungu wetu,
nitatafuta mafanikio yako.