Zaburi 123
Kuomba rehema 
 Wimbo wa kwenda juu. 
  1 Ninayainua macho yangu kwako,  
kwako wewe unayeketi mbinguni kwenye kiti chako cha enzi.   
 2 Kama vile macho ya watumwa  
yatazamavyo mkono wa bwana wao,  
kama vile macho ya mjakazi  
yatazamavyo mkono wa bibi yake,  
ndivyo macho yetu yamtazamavyo Mwenyezi Mungu, Mungu wetu,  
hadi atakapotuhurumia.   
 3 Uturehemu, Ee Mwenyezi Mungu, uturehemu,  
kwa maana tumevumilia dharau nyingi.   
 4 Tumevumilia dhihaka nyingi kutoka kwa wenye kiburi,  
dharau nyingi kutoka kwa wenye majivuno.