Zaburi 124
Shukrani kwa ukombozi wa Israeli
Wimbo wa kwenda juu. Wa Daudi.
1 Kama Mwenyezi Mungu hangekuwa upande wetu;
Israeli na aseme sasa:
2 kama Mwenyezi Mungu hangekuwa upande wetu,
watu walipotushambulia,
3 hasira yao ilipowaka dhidi yetu,
wangetumeza tukiwa hai,
4 mafuriko yangegharikisha,
maji mengi yangetufunika,
5 maji yaendayo kasi
yangetuchukua.
6 Ahimidiwe Mwenyezi Mungu,
ambaye hakuruhusu turaruliwe kwa meno yao.
7 Tumeponyoka kama ndege
kutoka mtego wa mwindaji;
mtego umevunjika,
nasi tumeokoka.
8 Msaada wetu ni katika jina la Mwenyezi Mungu,
Muumba wa mbingu na dunia.