Zaburi 124
Shukrani kwa ukombozi wa Israeli 
 Wimbo wa kwenda juu. Wa Daudi. 
  1 Kama Mwenyezi Mungu hangekuwa upande wetu;  
Israeli na aseme sasa:   
 2 kama Mwenyezi Mungu hangekuwa upande wetu,  
watu walipotushambulia,   
 3 hasira yao ilipowaka dhidi yetu,  
wangetumeza tukiwa hai,   
 4 mafuriko yangegharikisha,  
maji mengi yangetufunika,   
 5 maji yaendayo kasi  
yangetuchukua.   
 6 Ahimidiwe Mwenyezi Mungu,  
ambaye hakuruhusu turaruliwe kwa meno yao.   
 7 Tumeponyoka kama ndege  
kutoka mtego wa mwindaji;  
mtego umevunjika,  
nasi tumeokoka.   
 8 Msaada wetu ni katika jina la Mwenyezi Mungu,  
Muumba wa mbingu na dunia.