Zaburi 125
Usalama wa watu wa Mwenyezi Mungu
Wimbo wa kwenda juu.
1 Wale wamtumainio Mwenyezi Mungu ni kama Mlima Sayuni,
ambao hauwezi kutikisika, bali wadumu milele.
2 Kama milima inavyozunguka Yerusalemu,
ndivyo Mwenyezi Mungu anavyowazunguka watu wake
sasa na hata milele.
3 Fimbo ya waovu haitadumu juu ya nchi
waliyopewa wenye haki,
ili wenye haki wasije wakatumia
mikono yao kutenda ubaya.
4 Ee Mwenyezi Mungu, watendee mema walio wema,
wale walio wanyofu wa moyo.
5 Bali wale wanaogeukia njia zilizopotoka,
Mwenyezi Mungu atawafukuza pamoja na watenda maovu.
Amani iwe juu ya Israeli.