Zaburi 126
Kurejeshwa kutoka uhamisho 
 Wimbo wa kwenda juu. 
  1 Mwenyezi Mungu alipowarejesha mateka Sayuni,  
tulikuwa kama watu walioota ndoto.   
 2 Vinywa vyetu vilijaa kicheko,  
ndimi zetu zilijaa nyimbo za shangwe.  
Ndipo iliposemwa miongoni mwa mataifa,  
“Mwenyezi Mungu amewatendea mambo makuu.”   
 3 Mwenyezi Mungu ametutendea mambo makuu,  
nasi tumejaa furaha.   
 4 Ee Mwenyezi Mungu, turejeshee watu wetu waliotekwa,  
kama vijito katika Negebu.   
 5 Wapandao kwa machozi  
watavuna kwa nyimbo za shangwe.   
 6 Yeye azichukuaye mbegu zake  
kwenda kupanda, huku akilia,  
atarudi kwa nyimbo za shangwe,  
akichukua miganda ya mavuno yake.