Zaburi 126
Kurejeshwa kutoka uhamisho
Wimbo wa kwenda juu.
1 Mwenyezi Mungu alipowarejesha mateka Sayuni,
tulikuwa kama watu walioota ndoto.
2 Vinywa vyetu vilijaa kicheko,
ndimi zetu zilijaa nyimbo za shangwe.
Ndipo iliposemwa miongoni mwa mataifa,
“Mwenyezi Mungu amewatendea mambo makuu.”
3 Mwenyezi Mungu ametutendea mambo makuu,
nasi tumejaa furaha.
4 Ee Mwenyezi Mungu, turejeshee watu wetu waliotekwa,
kama vijito katika Negebu.
5 Wapandao kwa machozi
watavuna kwa nyimbo za shangwe.
6 Yeye azichukuaye mbegu zake
kwenda kupanda, huku akilia,
atarudi kwa nyimbo za shangwe,
akichukua miganda ya mavuno yake.