Zaburi 127
Bila Mwenyezi Mungu, kazi ya mwanadamu haifai 
 Wimbo wa kwenda juu. Wa Sulemani. 
  1 Mwenyezi Mungu asipoijenga nyumba,  
wajengao hufanya kazi bure.  
Mwenyezi Mungu asipoulinda mji,  
walinzi wakesha bure.   
 2 Mnajisumbua bure kuamka mapema  
na kuchelewa kulala,  
mkitaabikia chakula:  
kwa maana yeye huwapa usingizi wapendwa wake.   
 3 Watoto ni urithi unaotoka kwa Mwenyezi Mungu,  
uzao ni zawadi kutoka kwake.   
 4 Kama mishale mikononi mwa shujaa  
ndivyo walivyo wana awazaao mtu katika ujana wake.   
 5 Heri mtu ambaye podo lake  
limejazwa nao.  
Hawataaibishwa wanaposhindana  
na adui zao langoni.