Zaburi 128
Thawabu ya kumtii Mwenyezi Mungu 
 Wimbo wa kwenda juu. 
  1 Heri wale wote wamchao Mwenyezi Mungu,  
wanaoenda katika njia zake.   
 2 Utakula matunda ya kazi yako;  
baraka na mafanikio vitakuwa vyako.   
 3 Mke wako atakuwa kama mzabibu uzaao  
ndani ya nyumba yako;  
wana wako watakuwa kama machipukizi ya mizeituni  
kuizunguka meza yako.   
 4 Hivyo ndivyo atakavyobarikiwa  
mtu amchaye Mwenyezi Mungu.   
 5 Mwenyezi Mungu na akubariki kutoka Sayuni  
siku zote za maisha yako,  
na uone mafanikio ya Yerusalemu,   
 6 nawe ujaliwe kuishi uone watoto wa watoto wako.  
Amani iwe juu ya Israeli.