Zaburi 128
Thawabu ya kumtii Mwenyezi Mungu
Wimbo wa kwenda juu.
1 Heri wale wote wamchao Mwenyezi Mungu,
wanaoenda katika njia zake.
2 Utakula matunda ya kazi yako;
baraka na mafanikio vitakuwa vyako.
3 Mke wako atakuwa kama mzabibu uzaao
ndani ya nyumba yako;
wana wako watakuwa kama machipukizi ya mizeituni
kuizunguka meza yako.
4 Hivyo ndivyo atakavyobarikiwa
mtu amchaye Mwenyezi Mungu.
5 Mwenyezi Mungu na akubariki kutoka Sayuni
siku zote za maisha yako,
na uone mafanikio ya Yerusalemu,
6 nawe ujaliwe kuishi uone watoto wa watoto wako.
Amani iwe juu ya Israeli.