Zaburi 129
Maombi dhidi ya adui za Israeli 
 Wimbo wa kwenda juu. 
  1 Wamenitesa sana tangu ujana wangu;  
Israeli na aseme sasa:   
 2 wamenitesa sana tangu ujana wangu,  
lakini bado hawajanishinda.   
 3 Wakulima wamelima mgongo wangu,  
na kufanya mifereji yao mirefu.   
 4 Lakini Mwenyezi Mungu ni mwenye haki;  
amenifungua toka kamba za waovu.   
 5 Wale wote wanaoichukia Sayuni  
na warudishwe nyuma kwa aibu.   
 6 Wawe kama majani juu ya paa,  
ambayo hunyauka kabla hayajakua;   
 7 kwa hayo mvunaji hawezi kujaza vitanga vyake,  
wala akusanyaye kujaza mikono yake.   
 8 Wale wapitao karibu na wasiseme,  
“Baraka ya Mwenyezi Mungu iwe juu yako;  
tunakubariki katika jina la Mwenyezi Mungu.”