Zaburi 130
Kumngojea Mwenyezi Mungu 
 Wimbo wa kwenda juu. 
  1 Kutoka vilindini ninakulilia, Ee Mwenyezi Mungu.   
 2 Ee Bwana, sikia sauti yangu.  
Masikio yako na yawe masikivu  
kwa kilio changu unihurumie.   
 3 Kama wewe, Ee Mwenyezi Mungu, ungeweka kumbukumbu ya dhambi,  
Ee Bwana, ni nani angeweza kusimama?   
 4 Lakini kwako kuna msamaha,  
kwa hiyo wewe unaogopwa.   
 5 Namngojea Mwenyezi Mungu, nafsi yangu inangojea,  
katika neno lake naweka tumaini langu.   
 6 Nafsi yangu inamngojea Bwana  
kuliko walinzi waingojeavyo asubuhi,  
naam, kuliko walinzi  
waingojeavyo asubuhi.   
 7 Ee Israeli, mtumaini Mwenyezi Mungu,  
maana kwa Mwenyezi Mungu kuna upendo usiokoma,  
na kwake kuna ukombozi kamili.   
 8 Yeye mwenyewe ataikomboa Israeli  
kutoka dhambi zao zote.