Zaburi 130
Kumngojea Mwenyezi Mungu
Wimbo wa kwenda juu.
1 Kutoka vilindini ninakulilia, Ee Mwenyezi Mungu.
2 Ee Bwana, sikia sauti yangu.
Masikio yako na yawe masikivu
kwa kilio changu unihurumie.
3 Kama wewe, Ee Mwenyezi Mungu, ungeweka kumbukumbu ya dhambi,
Ee Bwana, ni nani angeweza kusimama?
4 Lakini kwako kuna msamaha,
kwa hiyo wewe unaogopwa.
5 Namngojea Mwenyezi Mungu, nafsi yangu inangojea,
katika neno lake naweka tumaini langu.
6 Nafsi yangu inamngojea Bwana
kuliko walinzi waingojeavyo asubuhi,
naam, kuliko walinzi
waingojeavyo asubuhi.
7 Ee Israeli, mtumaini Mwenyezi Mungu,
maana kwa Mwenyezi Mungu kuna upendo usiokoma,
na kwake kuna ukombozi kamili.
8 Yeye mwenyewe ataikomboa Israeli
kutoka dhambi zao zote.