Zaburi 138
Maombi ya shukrani 
 Zaburi ya Daudi. 
  1 Nitakusifu wewe, Ee Mwenyezi Mungu, kwa moyo wangu wote,  
mbele ya “miungu” nitaimba sifa zako.   
 2 Nitasujudu nikielekea Hekalu lako takatifu,  
nami nitalisifu jina lako  
kwa ajili ya upendo wako  
na uaminifu,  
kwa maana umeitukuza ahadi yako  
zaidi ya jina lako.   
 3 Nilipoita, ulinijibu;  
ulinifanya jasiri na mwenye moyo hodari.   
 4 Wafalme wote wa dunia wakusifu wewe Ee Mwenyezi Mungu,  
wakati wanaposikia maneno ya kinywa chako.   
 5 Wao na waimbe kuhusu njia za Mwenyezi Mungu,  
kwa maana utukufu wa Mwenyezi Mungu ni mkuu.   
 6 Ingawa Mwenyezi Mungu yuko juu,  
humwangalia mnyonge,  
bali mwenye kiburi  
yeye anamjua kutokea mbali.   
 7 Nijapopita katikati ya shida,  
wewe unayahifadhi maisha yangu,  
unanyoosha mkono wako dhidi ya hasira ya adui zangu,  
kwa mkono wako wa kuume unaniokoa.   
 8 Mwenyezi Mungu atatimiza kusudi lake kwangu,  
Ee Mwenyezi Mungu, upendo wako wadumu milele:  
usiziache kazi za mikono yako.