Zaburi 138
Maombi ya shukrani
Zaburi ya Daudi.
1 Nitakusifu wewe, Ee Mwenyezi Mungu, kwa moyo wangu wote,
mbele ya “miungu” nitaimba sifa zako.
2 Nitasujudu nikielekea Hekalu lako takatifu,
nami nitalisifu jina lako
kwa ajili ya upendo wako
na uaminifu,
kwa maana umeitukuza ahadi yako
zaidi ya jina lako.
3 Nilipoita, ulinijibu;
ulinifanya jasiri na mwenye moyo hodari.
4 Wafalme wote wa dunia wakusifu wewe Ee Mwenyezi Mungu,
wakati wanaposikia maneno ya kinywa chako.
5 Wao na waimbe kuhusu njia za Mwenyezi Mungu,
kwa maana utukufu wa Mwenyezi Mungu ni mkuu.
6 Ingawa Mwenyezi Mungu yuko juu,
humwangalia mnyonge,
bali mwenye kiburi
yeye anamjua kutokea mbali.
7 Nijapopita katikati ya shida,
wewe unayahifadhi maisha yangu,
unanyoosha mkono wako dhidi ya hasira ya adui zangu,
kwa mkono wako wa kuume unaniokoa.
8 Mwenyezi Mungu atatimiza kusudi lake kwangu,
Ee Mwenyezi Mungu, upendo wako wadumu milele:
usiziache kazi za mikono yako.