28
 1 Mtu mwovu hukimbia ingawa hakuna yeyote anayemfukuza,  
bali wenye haki ni wajasiri kama simba.   
 2 Nchi inapokuwa na uasi,  
inakuwa na viongozi wengi,  
bali kiongozi mwenye ufahamu na maarifa  
hudumisha utaratibu.   
 3 Mtawala anayewadhulumu maskini,  
ni kama mvua ya dhoruba inayoharibu mazao yote.   
 4 Wale wanaoacha sheria huwasifu waovu,  
bali wale wanaotii sheria huwapinga.   
 5 Wapotovu hawaelewi haki,  
bali wale wanaomtafuta Mwenyezi Mungu wanaielewa kikamilifu.   
 6 Afadhali maskini ambaye mwenendo wake hauna lawama,  
kuliko tajiri ambaye njia zake ni potovu.   
 7 Yeye anayetii sheria ni mwana mwenye ufahamu,  
bali rafiki wa walafi humwaibisha baba yake.   
 8 Yeye aongezaye utajiri wake kwa riba kubwa mno  
hukusanya kwa ajili ya mwingine,  
ambaye atawahurumia maskini.   
 9 Mtu yeyote akikataa kusikia sheria,  
hata maombi yake ni chukizo.   
 10 Yeye anayemwongoza mwenye haki kwenye mapito mabaya,  
ataanguka kwenye mtego wake mwenyewe,  
bali wasio na lawama watapokea urithi mwema.   
 11 Mtu tajiri anaweza kuwa na hekima machoni pake mwenyewe,  
bali mtu maskini mwenye busara  
humtambua alivyodanganyika.   
 12 Mwenye haki ashindapo, kuna furaha kubwa,  
bali waovu watawalapo, watu hujificha.   
 13 Yeye afichaye dhambi zake hatafanikiwa,  
bali yeyote aziungamaye na kuziacha hupata rehema.   
 14 Amebarikiwa mtu ambaye siku zote humcha Mwenyezi Mungu,  
bali yeye afanyaye moyo wake kuwa mgumu  
huanguka kwenye taabu.   
 15 Kama simba angurumaye au dubu ashambuliaye,  
ndivyo alivyo mtu mwovu anayetawala wanyonge.   
 16 Mtawala dhalimu hana akili,  
bali yeye achukiaye mapato ya udhalimu  
atafurahia maisha marefu.   
 17 Mtu mwenye kusumbuliwa na hatia ya kuua  
atakuwa mtoro hadi kufa;  
mtu yeyote asimsaidie.   
 18 Yeye ambaye mwenendo wake hauna lawama  
hulindwa salama,  
bali yeye ambaye njia zake ni potovu  
ataanguka ghafula.   
 19 Yeye alimaye shamba lake atakuwa na chakula tele,  
bali yule afuataye mambo ya upuzi atakuwa na umaskini wa kumtosha.   
 20 Mtu mwaminifu atabarikiwa sana,  
bali yeye atamaniye kupata utajiri kwa haraka  
hataacha kuadhibiwa.   
 21 Kuonesha upendeleo si vizuri,  
hata hivyo mtu atafanya kosa kwa kipande cha mkate.   
 22 Mtu mchoyo ana tamaa ya kupata utajiri,  
naye hana habari kuwa umaskini unamngojea.   
 23 Yeye amkemeaye mtu mwishoni hupata kibali zaidi,  
kuliko mwenye maneno ya kusifu isivyostahili.   
 24 Yeye amwibiaye babaye au mamaye  
na kusema, “Si kosa,”  
yeye ni mwenzi wa yule aharibuye.   
 25 Mtu mwenye tamaa huchochea fitina,  
bali yule amtegemeaye Mwenyezi Mungu atafanikiwa.   
 26 Yeye ajitumainiaye mwenyewe ni mpumbavu,  
bali yeye atembeaye katika hekima hulindwa salama.   
 27 Yeye ampaye maskini  
hatapungukiwa na kitu chochote,  
bali yeye awafumbiaye maskini macho  
hupata laana nyingi.   
 28 Wakati waovu wanatawala,  
watu huenda mafichoni,  
bali waovu wanapoangamia,  
wenye haki hufanikiwa.