Zaburi 47
Mtawala mwenye enzi yote 
 Kwa mwimbishaji. Zaburi ya wana wa Kora. 
  1 Pigeni makofi, enyi mataifa yote,  
mpigieni Mungu kelele za shangwe!   
 2 Jinsi gani alivyo wa kutisha, Mwenyezi Mungu Aliye Juu Sana,  
Mfalme mkuu juu ya dunia yote!   
 3 Ametiisha mataifa chini yetu,  
watu wengi chini ya miguu yetu.   
 4 Alituchagulia urithi wetu,  
fahari ya Yakobo, aliyempenda.   
 5 Mungu amepaa kwa kelele za shangwe,  
Mwenyezi Mungu kwa sauti za tarumbeta.   
 6 Mwimbieni Mungu sifa, imbeni sifa,  
mwimbieni sifa Mfalme wetu, imbeni sifa.   
 7 Kwa kuwa Mungu ni mfalme wa dunia yote,  
mwimbieni zaburi za sifa.   
 8 Mungu anayatawala mataifa,  
Mungu ameketi kwenye kiti chake cha enzi kitakatifu.   
 9 Wakuu wa mataifa wanakusanyika  
kama watu wa Mungu wa Ibrahimu,  
kwa kuwa wafalme wa dunia ni mali ya Mungu;  
yeye ametukuka sana.