Zaburi 111
Sifa za Mwenyezi Mungu kwa matendo ya ajabu 
  1 Msifuni Mwenyezi Mungu.†kwa Kiebrania ni Hallelu Yah.  
Nitamtukuza Mwenyezi Mungu kwa moyo wangu wote,  
katika baraza la wanyofu na katika kusanyiko.   
 2 Kazi za Mwenyezi Mungu ni kuu,  
wote wanaopendezwa nazo huzitafakari.   
 3 Kazi zake zimejaa fahari na utukufu,  
haki yake hudumu daima.   
 4 Amefanya maajabu yake yakumbukwe,  
Mwenyezi Mungu ni mwenye neema na huruma.   
 5 Huwapa chakula wale wanaomcha,  
hulikumbuka agano lake milele.   
 6 Amewaonesha watu wake uwezo wa kazi zake,  
akiwapa nchi za mataifa mengine.   
 7 Kazi za mikono yake ni za uaminifu na haki,  
mausia yake yote ni ya kuaminika.   
 8 Zinadumu milele na milele,  
zikifanyika kwa uaminifu na unyofu.   
 9 Aliwapa watu wake ukombozi,  
aliamuru agano lake milele:  
jina lake ni takatifu na la kuogopwa.   
 10 Kumcha Mwenyezi Mungu ndicho chanzo cha hekima,  
wote wanaozifuata amri zake wana busara.  
Sifa zake zadumu milele.   
*^ Zaburi hii imetungwa kila mstari ukianzia na herufi ya alfabeti ya Kiebrania zikifuatana tangu Aleph (A) hadi Taw (T); zote ni 22.
†Zaburi 111:1 kwa Kiebrania ni Hallelu Yah.