Zaburi 113
Kumsifu Mwenyezi Mungu kwa wema wake
Msifuni Mwenyezi Mungu.*kwa Kiebrania ni Hallelu Yah; pia 113:9.
 
Enyi watumishi wa Mwenyezi Mungu msifuni,
lisifuni jina la Mwenyezi Mungu.
Jina la Mwenyezi Mungu na lisifiwe,
sasa na hata milele.
Kuanzia mawio ya jua hadi machweo yake,
jina la Mwenyezi Mungu linapaswa kusifiwa.
 
Mwenyezi Mungu ametukuka juu ya mataifa yote,
utukufu wake juu ya mbingu.
Ni nani aliye kama Mwenyezi Mungu, Mungu wetu,
Yule aliyeketi kwenye kiti cha enzi huko juu,
ambaye huinama atazame chini
aone mbingu na nchi?
 
Huwainua maskini kutoka mavumbini,
na kuwanyanyua wahitaji
kutoka lundo la majivu,
huwaketisha pamoja na wakuu,
pamoja na wakuu wa watu wake.
Humjalia mwanamke tasa kutulia nyumbani mwake,
akiwa mama watoto mwenye furaha.
 
Msifuni Mwenyezi Mungu.

*Zaburi 113:1 kwa Kiebrania ni Hallelu Yah; pia 113:9.