Zaburi 149
Wimbo wa kumsifu Mwenyezi Mungu kwa wema wake 
  1 Msifuni Mwenyezi Mungu.*kwa Kiebrania ni Hallelu Yah; pia 149:9.  
Mwimbieni Mwenyezi Mungu wimbo mpya,  
sifa zake katika kusanyiko la watakatifu.   
 2 Israeli na washangilie katika Muumba wao,  
watu wa Sayuni na wafurahi katika Mfalme wao.   
 3 Na walisifu jina lake kwa kucheza  
na wampigie muziki kwa matari na kinubi.   
 4 Kwa maana Mwenyezi Mungu anapendezwa na watu wake,  
anawavika wanyenyekevu taji la wokovu.   
 5 Watakatifu washangilie katika heshima hii,  
na waimbe kwa shangwe vitandani mwao.   
 6 Sifa za Mungu na ziwe vinywani mwao  
na upanga ukatao kuwili mikononi mwao,   
 7 ili walipize mataifa kisasi  
na adhabu juu ya mataifa,   
 8 wawafunge wafalme wao kwa minyororo,  
wakuu wao kwa pingu za chuma,   
 9 ili kuwafanyia hukumu iliyoandikwa dhidi yao.  
Huu ndio utukufu wa watakatifu wake wote.  
Msifuni Mwenyezi Mungu.